Adhabu ya jino kwa jino na Musitakabali wa imani zetu Nabii Musa alipotoka mlima Sinai kupewa amri kumi za Mungu zilizoko kwenye kitabu cha Kutoka 20:1 17, Mungu alimpa na sharia zingine ambazo lengo lake lilikuwa kumsaidia kutawala na kuamua kesi za kiraia za wana wa Israel. Kwa hiyo Mungu alimpa Musa sharia za aina nne. Naomba katika kueleweshana tupitie makundi haya manne ya sharia ambazo Mungu alimpa Musa, maana yake na utekelezaji wake. Kundi la kwanza la sharia: Sheria Takatifu ya Amri Kumi za Mungu Moral laws Hizi ni amri Kumi takatifu za Mungu ambazo Mungu aliziandika kwa mkono wake kwenye mbao mbili za mawe. Mungu aliandika mwenyewe kwa chanda chake! Haya si maneno yangu. Katika kitabu cha Kumbukumbu la torati 5:22 anasema hivi: Haya ndiyo maneno ambayo Bwana aliwaambia mkutano wenu wote mlimani kwa sauti kuu toka kati ya moto, na wingu, na giza kuu; wala hakuongeza neno. Akayaandika juu ya mbao mbili za mawe, akanipa. Kuna sehemu tatu mimi ninazozijua ambazo Mungu aliandika maneno yake yeye mwenyewe hakutumia nabii. Sitazisema zote kwa sasa kwa sababu ya muda. Ila tu cha msingi kwetu sisi wanadamu ni kuelewa umuhimu wa kitu ambacho Mungu alikiandika mwenyewe. Mungu aliandika Amri kumi katika mbao mbili za mawe akamkabidhi Musa awapatie wana wa Israel. Kama nilivyoeleza hapo mwanzo amri kumi ni takatifu na hazibadiliki. Lengo la amri hizi ni kuweka kanuni ya namna sisi wanadamu tunavyopaswa kuhusiana na Mungu Muumbaji. Ukizipitia kwa haraka Amri nne za mwanzo: 1.Usiwe na miungu mingine ila mimi 2. Usijifanyia sana ya kuchonga na kuisujudia, 3. Usiliataje bure jina la Mungu, 4. Ikumbuke siku ya Sabato uitakase, siku hiyo usifanye kazi yoyote Utagundua kwamba kwa ujumla wake Zinaweka msingi wa namna ya kuhusiana na Mungu wetu Muumbaji. Zote hizi zimejumuishwa katia amri ile kuu ya kwanza ambayo Mungu alimwambia Musa katika kitabu cha: Kumb 6:3-5 3 Sikiza basi, Ee Israeli, ukaangalie kuzitenda; upate kufanikiwa, mpate kuongezeka sana, kama Bwana, Mungu wa baba zako, alivyokuahidi, katika nchi ijaayo maziwa na asali. 4 Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. 5 Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote. Maana yake ni rahisi tu, ukimpenda Mungu wako Muumbaji huwezi kuwa na miungu wengine, hutachongo sanamu na kuiabudu, hutalitaja jina lake bure na hutaivunja wala kuiponda sabato yake utaitumia kumwabudu yeye peke yake.
Habari gani juu ya Amri sita za mwisho? Hizi Amri huweka msingi wa mahusiano kati ya binadamu na binadamu. Yaani sisi wanadamu tutaishije, tutatendeanaje? Hebu iangalie orodha ya hizi sita kwa ufupi Kutoka 20:12-17 5. Waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako. 6. Usiue. 7. Usizini. 8. Usiibe. 9. Usimshuhudie jirani yako uongo. 10. Usiitamani nyumba ya jirani yako, usimtamani mke wa jirani yako; wala mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala ng'ombe wake, wala punda wake, wala cho chote alicho nacho jirani yako. Hizi Zinajumuishwa na Amri kuu ya pili isemayo Mpende Jirani yako kama nafsi yako, Mathayo 22:39. Ukimpenda jirani yako huwezi kumuua, huwezi kuzini na binti yake au mke wake, huwezi kumwibia, huwezi kumshuhudia uongo, huwezi kutamani nyumba yake, mke wake wala mali zake. Baba yako na mama yako Je? Hapo ndipo kwenye kiini cha mahusiano. Huo ndio mtiririko wa Amri takatifu. Hizi hazibadiriki ni sharia ya milele ya Mungu. Ukitaka upate matatizo hapa dunia hata leo jaribu kuchezea moja katika hizo utaona kitachokupata. Ndiyo maana mtume Yakobo katika sura ya 2: 9,10 anasema: 9 Maana mtu awaye yote atakayeishika sheria yote, ila akajikwaa katika neno moja, amekosa juu ya yote. 10 Kwa maana yeye aliyesema, Usizini, pia alisema, Usiue. Basi ijapokuwa hukuzini, lakini umeua, umekuwa mvunja sheria. Kuna watu wamefundisha kuwa Amri kumi za Mungu zilifutwa na Yesu alipokuja. Hii si kweli hata kidogo. Yesu mwenyewe anasema katika kitabu cha Mathayo 5: 17 19: 17 Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. 18 Kwa maana, amin, nawaambia,mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka,yodi moja wala nukta moja ya torati haitaoondoka,hata yote yatimie. 19 Basi mtu ye yote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni. Kwa hiyo Yesu hakutengua torati hata moja, alikuja kuitimiza. Na ndiyo maana hata katika kitabu cha Luka 4:16 Yesu alitunza hata sabato yenyewe ambayo siku hizi wakristo tunapata kigugumizi kuwaambia waumini juu ya ukweli huu. 16 Akaenda Nazareti, hapo alipolelewa; na siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi yake, akasimama ili asome. Usichoke rafiki yangu sasa tunaingia kundi la pili la sharia:
Kundi la pili la sharia: Sheria ya kitaifa yaani civil laws Hizi ni taratibu ambazo Mungu alimpatia Musa kuongoza wana wa Israeli kama taifa. Tukumbuke Musa alikiwa kiongozi wa kidini lakini pia wa kitaifa. Hivyo Mungu alimpa kanuni za namna ya kuamua kesi mbali mbali za maisha ya raia wa Israeli kutawala mahusiano ya kimaisha na kisiasa ya kila siku. Sheria hizo zimeandikwa katika kitabu cha Kutoka 21 23. Zilitawala maisha ya kila siku na zilionyesha utaratibu wa kuamua kesi na makosa. Pia sharia hizi zilielekeza adhabu ya kutoa kwa wakosaji. Hapa ndipo tunakuta kiini cha kanuni ya adhabu ya jino kwa jino ambayo ndiyo imenisababisha niandike makala hii ya msingi sana kuona je, matumizi ya adhabu hii kama inavyodaiwa na baadhi ya wanazuoni na watoa mihadhara ni sahihi? Kanuni hii inapatikana katika kitabu cha Kutoka 21: 22 25 inasema: 22 Watu waume wakiteta pamoja, wakamwumiza mwanamke mwenye mimba hata akaharibu mimba, tena yasiwe madhara zaidi; sharti atatozwa mali kama atakavyomwandikia mumewe huyo mwanamke; atalipa kama hao waamuzi watakavyosema. 23 Lakini kwamba pana madhara zaidi, ndipo utatoza uhai kwa uhai, 24 jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu, 25 kuteketeza kwa kuteketeza, jeraha kwa jeraha, chubuko kwa ajili ya chubuko. Kanuni hii iliwekwa kuongoza waamuzi namna ya kutoa adhabu kwa wakosaji. Kwanza kabisa ilipaswa kutekeleza katika mazingira ya fungu la 22 nadhani hii iko wazi. Ukiendelea kusoma zaidi hasa Kutoka 21:12 anasema: 12 Mtu awaye yote ampigaye mtu, hata akafa, hana budi atauawa huyo. Hii ilikuwa ni adhabu ya moja kwa moja kwa mhusika ambayo nadhani hata leo baadhi ya mataifa tunaitumia. Adhabu hii haikutekelezwa kwa mazingira ya kwamba mtu yeyote anaweza kuitekeleza kwa mtu yeyote aliyeua. La hasha, ilikuwa lazima ushahidi upitiwe na maamuzi ya haki yatolewe. Leo unamsikia mtoa mhadhara anasema lazima kulipiza kisasi, kwa nani? kwa mtu yeyote kweli? Polisi wanatuliza ghasia mahali, wanaua muumini wa dini fulani halafu mfuasi mwingine wa dini hiyo anaenda kuua kiongozi wa dini nyingine! Nina hakika kwa sababu torati ya Musa ndiyo ile ile ya Kuruani ni makosa kufanya hivyo. Kama una muda soma sura hizi tatu fuatilia na Kuruani inavyosema vinafanana kwa kiasi fulani. Jino kwa jino haiendi kwa mtu yeyote bali tu kwa mhusika alotenda kosa. Hata hivyo Serikali ni mamlaka ambayo Misahafu yote inasema iheshimiwe. Kama polisi ametekeleza kazi yake vibaya hadi akaua, kuna sharia ya kumhukumu na kama ni makusudi adhabu yake huishia kwenye jino kwa jino yaani na yeye kuuawa. Kwa hivyo si sahihi muumini wa kiislamu kuondoka kwenda kuua tu mtu yeyote ili muradi anatimiza hasira yake kwa mwenzake aliyeuawa na mtu mwingine kabisa. Nchi zinazotawaliwa kiislam wanatumi sharia na vitu hivi viko wazi sana na utekelezaji wa adhabu unafuata vizuri maelekezo ya kanuni hizi za adhabu.
Je hizi sharia za kiraia zinaendelea kufanya kazi? Kwa wakristo taifa la Israeli lilikoma kuwa taifa takatifu la Mungu mwaka 70AD walipofanya kila juhudi ya kumkataa Yesu. Nahivyo mitume wakawageukia mataifa kueneza injili na ndipo sasa mataifa yote wakimwamini Kristo wanakuwa uzao wa Ibrahim. Sheria hizi hazitumiki tena. Na sababu ni rahisi tu kila taifa lina sharia zake za kiraia zinazotungwa na mabunge. Zile ziliwekwa kumsaidia Musa kuongoza wana wa Israeli. Kwa namna kubwa sharia nyingi za nchi zimejengwa katika misingi hii. Kundi la tatu la sharia: Sheria ya ibada ya patakatifu Ceremonial laws Hizi tunazipata katika kitabu cha Kutoka 30, na hasa Kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 1 9. Sharia hizi zinazungumzia utaratibu wa ibada. Namna ya kupataniswa na Mungu unapotenda makosa, dhambi na uasi. Kuanzia Adamu na Hawa walipotenda dhambi hadi wakati wa Yesu akingali hai, wanadamu waliagizwa na Mungu kutoa sadaka ya kafara ya dhambi ili waweze kusamehewa makosa, dhambi na uasi wao. Mungu alimwamuru Musa ajenge patakatifu ambapo ibada hizi zilifanyika. Hekalu hili lilikuwa na sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ambapo ibada za kila siku zilifanyika. Mwenye dhambi ama mkosaji alikuja na sadaka ya mnyama ili achinjwe na kuchomwa kwa ajili yake. Maana yake ilikuwa kwamba yule mkosaji alipaswa kufa lakini badala yake mnyama alikufa kwa ajili yake. Hekalu na taratibu zake zilihudumiwa na watumishi waliokuwa wakiitwa Makuhani iliyotokana kabila ya Walawi katika Israeli. Nimezungumzia sehemu ya kwanza ya hekalu. Sehemu ya pili ilikuwa inaitwa patakatifu mno au patakatifu pa patakatifu. Sehemu hii Kuhani mkuu aliingia mara moja tu kwa mwaka. Siku hii ilikuwa sikukuu kwa wana wa Israeli. Iliitwa siku ya upanisho kwa Kiebrania ilijulikana kama Yom Kipur au kwa kiingereza The day of Atonenment. Hii ilikuwa siku maalumu ya kutakasa hekalu kutokana na dhambi za mwaka mzima zilizopelekwa pale na wakosaji. Ilitakiwa mara moja kwa mwaka hekalu litakaswe yaani lisafishwe. Siku hii kuhani aliingia mara moja kwenye sehemu hii ya patakatifu kuwakilisha Taifa zima la Israeli. Semu hii ilikuwa takatifu mno, hakuna mtu aliyerusiwa na Mungu kuingia wala kuona sehemu hii ya pili isipokuwa Kuhani Mkuu peke yake naye mara moja kwa mwaka. Hata Kuhani Mkuu ilibidi ajitakase na akienda huko alifungwa kamba ili ikitokea hakujikasa akakutana na utukufu wa Mungu akafa muweza kumvuta na hiyo kamba. Yote haya unayapata katika vitabu nilivyovitaja hapo juu, si maneno yangu. Pale patakatifu pa patakatifu kulikuwa na sanduku la agano ambalo ndani yake zile mbao mbili za mawe zilizokuwa zimeandikwa amri kumi za Mungu ziliwekwa kwenye sanduku hili. Halafu pembeni lilikingwa na Makerubi wawili walioinua mabawa yao yakikutana kwa juu. Ilikuwa sehemu iliyowakilisha kiti cha enzi cha Mungu ikiwakilisha uwepo wake katikati ya watu wake. Kwa hiyo Mungu aliweka taratibu mbalimbali kama sharia za huduma za mahali hapa, ikihusisha usafi wa mwili (kama kutawadha miguu), utoaji wa dhabihu na kadhalika. Je hizi sharia za ibada za patakatifu na taratibu zake zinaendelea kufanya kazi? Somo la patakatifu ni refu sana lakini kwa ujumla wake sadaka hizi za kuteketezwa na huduma zote za patakatifu yaani hekalu zilikuwa ni kivuli cha sadaka halisi ya Yesu Kristo ambaye alkuja akafa
msalabani kwa ajili ya watu wote. Na hivyo ibada ya kutoa kafara wanyama ikakoma maana kafara kuu ambayo ni Yesu ilitolewa na Mungu Mwenyewe. Siku Yesu alipokufa msalabani palitokea jambo la ajabu sana. Ujue ilikuwa ni saa za alasiri na kule Yerusalem Wayahudi wengine walikuwa hekaluni wakitoa kafara. Ghafla ikawa giza na tetemeko kuu, miamba ikapasuka na Mathayo 27:51 inasema pazia la hekalu, yaani lile lililotenganisha patakatifu na patakatifu pa patakatifu likapasuka, kondoo aliyekuwa kwenye madhabahu tayari kuchinjwa kama kafara akakimbia. Kwa mara ya kwanza waabudu waliokuwepo siku ile hekaluni wakaona kwa macho yao sehemu hii ya patakatifu pa patakatifu na wala hawakudhurika. Kwa namna ya pekee kifo cha Yesu kikakomesha ibada hii ya patakatifu na mambo yote ya kafara. Sheria hizi za patakatifu hazitumiki tena ziliisha pale Yesu alipokufa masalabani kama kafara kuu ya wanadamu wote. Na ndiyo maana anasema kila amwaniye ataokoka. Hana ubaguzi. Damu yake ilimwagika kwa ajili ya wanadamu wote. Kundi la nne la sharia: Sheria ya afya au zaidi sharia ya vyakula Dietary laws Hii kwa ujumla inapatikana sehemu mbali mbali za Biblia lakini msingi wake ni katika kitabu cha Mambo ya Walawi sura ya 11: 1-47. Katika aya hizi Mungu alitoa kanuni ya ulaji kwa wana wa Isael. Na sehemu zingine katika Biblia Alitoa kanuni za usafi, matumizi ya vyoo, kutahiri na mambo mengi ya afya. Wanyama wachafu kama nguruwe na wengineo waliotajwa Mungu aliwakataza wana wa Israel kula nyama na damu yake. Aliweka kanuni ya kuchagua viumbe wanaofaa kuliwa na wasiofaa. Kanuni hizi zilihusisha makundi yote ikiwemo viumbe wa nchi kavu na majini, wanaoruka na wasiruka na kadhalika. Mungu alitoa kanuni ya hali ya juu sana ya kuzingatia afya. Dini nyingi sana zimejikwaa katika sharia hii. Wengine wamefuata sharia hii kwa ukamilifu wake, wengine wanachagua na kukubali kutokula baadhi ya wanyama na samaki waliokatazwa lakini wengine wanawala. Wengine wanaipinga sharia yote wakidai Yesu aliruhusu watu wale kila kitu. Mnyama anayeshindaniwa sana ni nguruwe. Ushindani umelenga sana huyu mnyama hadi tumesahau kwamba kuna wanyama wengine pia ni haramu wakiwemo punda, ngamia, mbwa, na jinsi zao zote. Nguruwe ni haramu lakini pia wanyama wanye sifa kama zake ni haramu pia. Samaki wasio na magamba au mapezi ni haramu kwa mujibu wa sharia hii. Kuna viumbe wengine majini hata si samaki lakini binadamu wanawala unashangaa inakuwaje. Tunapata kigugumizi kutimiza tamaa ya mwili na si mapenzi ya Mungu. Viumbe vingine Mungu aliviweka kama mabwana afya wa mazingira lakini navyo tunavila. Ndiyo maana tunapambana na uchafu ambao huenda ungepunguzwa na hawa viumbe tuliowageuza vitoweo. Kimsingi nyama hakikuwa chakula cha mwanzo cha binadamu. Mungu alikuja kuongezea na kuruhusu tule nyama baada ya gharika ya Nuhu. Hata hivyo Mungu aliruhusu kwa tahadhari kubwa kwa mfano alisema: - Tusile nyama na damu yake (mnyama lazima achinjwe kutenganisha damu na nyama yake). Mungu alikuwa na maana yake. - Alikataza kula wanyama waliokufa kibudu hii hata leo bado ni hatari. - Alikataza kula mafuta na matumbo najua wengi tunapenda kisusio - Alikataza kula damu ndugu zangu wamasai watalalamika lakini Mungu anajua madhara yake. Leo wataalamu wanajua magonjwa yote hutembea katika damu. Ndiyo maana magonjwa yote huwa tunapima damu maana ndiko wadudu hukaa. - Aliagiza nyama ikaushwe - Na kadhalika
Kwa ujumla nyama inatakiwa iliwe kwa uangalifu na ikiwezakana kama kuna mbadala wa protini iachwe kabisa. Je hizi sharia afya na taratibu zake zinaendelea kufanya kazi? Jibu tunalipata katika kitabu cha 1 Kor 6:18-20 18 Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe; 19 maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu. Sheria za afya bado ni valid yaani bado zinahitajika kwa ustawi na maisha bora. Tusiingize vitu vichafu mwilini na tusiutendee mwili mambo yasiyo faa. Hitimisho (Conclusion) Kwa hivyo ndugu zangu Sheria ya Amri kumi za Mungu ni takatifu na ndiyo kiwango ambacho Mungu atauhukumu ulimwengu kwazo. They are immutable hazitabadilika. Sote tunapimwa kwa hizo. Sheria ya kiraia na ile ya ibada za patakatifu ilikoma baada ya kifo cha Yesu Msalabani. Japo kwa namna Fulani sharia za kiraia ambazo zilitoa utaratibu wa kushughulika na makosa ya jinai, makosa ya zinaa, na torts bado leo zimejenga misingi ya sharia mbali mbali za nchi. Hazina ubaya kutumika lakini si sehemu ya ibada kwa waumini. Sheria za afya ni muhimu na kwa sababu mwili wa mwanadamu ni ule ule na unahitaji afya taratibu hizi za ulaji, mazingira na afya kwa ujumla bado zinatenda kazi. Tukizifuata tutapunguza magonjwa na vifo vya kabla ya wakati. Tutumie maandiko ya Biblia na Quran kwa busara tukimwomba Mungu atutafsirie yaliyoko humu tulete amani na upendo kati yetu tukihurumiana na kutendeana kwa wema. Wakosaji pia ni watu wa Mungu tuwatendee kwa haki tukizingatia Mungu alivotuagiza na kuheshimu mamlaka ya nchi ambayo ni halali na haiendi kinyume cha maelekezo ya Mwenyezi Mungu. Tutendeane kwa haki tukifuata amani, upendo na sharia. Mbarikiwe sana Mliosoma makala hii. Nitaitafsiri kwa kiingereza kwa wale ambao hawakuelewa mjadala huu (I ll shortly translate the article into English for those who did not follow the discussion in Swahili). Natoa shukurani kwa Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kutoa makala hii, ni matumaini yangu kuwa itamsaidia mtu fulani. Mada inayofuata tutazungumzia uchinjaji wa wanyama kwa ajili ya chakula.