KIJARIDA JUU YA HAKI ZA RAIA KATIKA MFUMO JINAI KIMETOLEWA NA CHAMA CHA WANASHERIA TANZANIA BARA KWA UFADHILI WA TAASISI YA LEGAL SERVICE FACILITY (LSF) 1
KIMEANDALIWA NA Chama Cha Wanasheria Tanzania Bara Kiwanja Na. 391, Mtaa wa Chato Regent Estate, S.L.P 2148 Dar es Salaam, Tanzania. Simu +255 22 2775313/ +255 22 5500002 Nukushi +255 22 2775314 Barua Pepe info@tls.or.tz Tovuti www.tls.or.tz Chama Cha Wanasheria Tanzania Bara, 2015 Waandishi Jane Salomo Kaleb Gamaya Scholastica Jullu Wahariri Mercy Kessy Stephen Msechu John Mwangombola Magdalena A. Mlolere Fortunata Kitokesya Said Chitung Ramadhan Masele Saada Mkangwa 1
Kimeandikwa na kuhaririwa chini ya usimamizi wa; Kamati ya Msaada wa Sheria Anna Kulaya-Mwenyekiti Butamo Philip Daniel Lema Donesta Byarugaba Fulgence Massawe Maria Matui Kamati ya Utafiti na Machapisho Prof. Cyriacus Binamungu Dr. Alex Makuklilo Dr. Lilian Mongela Elifuraha Laltaika Madeline Kimei Nuhu Mkumbukwa 2
SHUKRANI Kamati ya Msaada wa Sheria Tanzania Bara kwa niaba ya Baraza la Uongozi la Chama inatoa shukrani za dhati kwa Kamati ya Utafiti na Machapisho ya Chama cha Wanasheria Tanzania Bara na shirika la Legal Service Facilities kwa kushiriki kikamilifu katika hatua mbalimbali za kuandaa kijarida hiki. Kwa namna ya pekee, kamati inaishukuru Sekretariat ya Chama cha Wanasheria Tanzania Bara kwa kazi kubwa walioifanya katika kufanikisha uandikishaji wa kijarida hiki. Lengo la kijarida Kijarida hiki kimeandaliwa kwa lengo la kuielimisha jamii kuhusu haki za raia katika mfumo wa jinai nchini Tanzania.Msomaji atapata kuelewa Maana ya jinai na tofauti kati ya Jinai na Madai. Sababu za Jamhuri Kuendesha Mashauri ya Jinai Taratibu za kumtia nguvuni mtuhumiwa Haki na utaratibu wa Kupata Dhamana Mamlaka ya Jeshi la Polisi katika Mfumo Jinai Haki za Msingi kwa Raia Katika Makosa ya Jinai Taratibu za Kukamatwa hadi Kuendesha Mashauri ya Jinai Jinsi ya Kufanya Upekuzi Usikilizaji wa Mashitaka ya Jinai Mahakamani Adhabu Katika Makosa ya Jinai Hatua za kuchukua mshtakiwa asiporidhika na hukumu 3
JInai 1.0 Maana ya Jinai Jinai ni kosa au makosa yanayofanywa na mtu/watu/ taasisi kupitia watendaji wake, kinyume cha sheria au taratibu zilizoainisha makosa mbali mbali. Kwa mfano, makosa yote yaliyoainishwa katika Sheria ya Kanuni za Adhabu Sura ya 16 (the Penal Code), iliyopo katika orodha ya sheria za Tanzania. Tofauti kati ya Jinai na madai ni kwamba, kosa la jinai huhesabiwa ni kosa dhidi ya Jamhuri na madai ni lalamiko dhidi ya mtu binafsi, kampuni, taasisi au serikali kutokana na makubaliano fulani. 1.1 Tofauti Kati ya Jinai na Madai Jinai Madai 1. Kosa hutajwa katika Sheria Madai hutokana na za Kanuni za Adhabu kutoelewana kwa pande mbili katika makubaliano fulani. 2. Mlalamikiwa anaweza kukamatwa na vyombo vya dola au mtu yeyote na kutiwa nguvuni mpaka pale atakapopata dhamana Mlalamikaji peke yake anaweza kufikisha lalamiko lake mbele ya vyombo vya maamuzi. 4
3. Mlalamikaji ni Jamhuri (polisi, TAKUKURU, Mwendesha Mashitaka, au Mwanasheria wa Serikali, kwa niaba ya mtendewa kosa). 5 Mlalamikaji yeye mwenyewe au kupitia wakili wake ni mdaawa katika makubaliano 4. Utekelezaji wa kanuni, sheria Utekelezaji wa makubaliano na taratibu hufanywa na vyombo hufanywa na wadaawa wa vya dola ambavyo ni mgambo au mkataba au makubaliano. sungusungu, polisi, TAKUKURU, Usalama wa Taifa na serikali 5. Mshitakiwa au mwenye Mdaawa aliyekiuka hatia katika kosa hukabiliwa na makubaliano hulazimika adhabu ya ama onyo, viboko, kutekeleza makubaliano faini, kifungo n.k 6. Mshitakiwa ni yule aliyetenda kitendo cha jinai, aliyesaidia kutendeka kwa kosa la jinai, aliyeshawishi kutendeka kwa koa la jinai au aliyekwepa kuzuia kutotendeka kwa kosa la jinai, Ni mdaawa au mwathirika aliye kwenye makubaliano Sababu za Jamhuri Kuendesha Mashauri ya Jinai i. Jamhuri ina dhamana na wajibu wa kuhifadhi na kulinda raia na mali zao dhidi ya wahalifu. ii. Baadhi ya makosa ya jinai hayana madhara ya moja kwa moja kwa mtu binafsi na hivyo kukosekana kwa mtu ambaye ana nia na yuko tayari kufungua mashitaka dhidi ya mtuhumiwa. iii. Makosa mengine ya jinai kama vile mauaji ni mazito
kwa mtendewa na hata kwa jamii nzima. iv. Makosa ya jinai hujumuisha adhabu ikiwa ni pamoja na mifungo. v. Makosa ya jinai yanahitaji gharama kubwa kwa mfano; kuchunguza, kuendesha mashitaka na kutunza watuhumiwa na baadae wafungwa. UKAMATAJI MTUHUMIWA Taratibu za kumtia nguvuni mtuhumiwa Kuna taratibu mbili za kumtia nguvuni mtuhumiwa. Nazo ni: Ukamataji kwa Kutumia Hati Hati ya ukamataji ni hati inayotoa amri ya kukamatwa mtuhumiwa wa jinai. Hati hii inaweza kutolewa na vyombo mbali mbali ikiwamo polisi, mlinzi wa amani (mtendaji wa kijiji au kata), hakimu na jaji. Hati ya kukamata inapaswa iwe na vitu vifuavyo:- (i) Iwe imetolewa na Mkuu wa Kituo cha polisi, hakimu au mtendaji; (ii) Lazima iwe na mhuri wa polisi, mahakama au mtendaji; (iii) Iwe imesainiwa; (iv) Lazima iwe na maelezo ya mtuhumiwa kama vile Jina, kabila na dini. (v) Ielezee tuhuma na sababu za kukamatwa na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria kujibu tuhuma. 6
Ukamataji bila Kuwa na Hati Mtu yeyeote anaweza kumkamata mtuhumiwa bila kuwa na hati ya ukamataji baada ya mtuhumiwa kuonekana ametenda kosa la jinai. Mazingira ya Ukamataji bila Kuwa na Hati ya Ukamataji Mazingira yafuatayo yanampatia mtu binafsi au askari polisi haki ya kumkamata mtuhumiwa bila ya kuwa na hati ya kukamata. i) mtu atafanya tendo la kuvunja amani mbele ya askari, ii) mtu atamzuia askari polisi kufanya kazi zake, au atafanya jaribio la kutoroka au atatoroka kutoka chini ya ulinzi, iii) mtu ataonekana kuwa na mali ya wizi au inayoshukiwa kuwa ya wizi, iv) mzururaji au mtu anayezurura kwa nia ya kufanya uhalifu, v) mtu anayehisiwa kuwa hati ya kukamatwa vi) imeshatolewa dhidi yake, mtu yeyote ambaye amefanya kosa nje ya Tanzania na kuna uwezekano wa kuadhibiwa ndani ya Tanzania, vii) mtu anayedharau nembo ya taifa kama vile wimbo wa Taifa au Bendera ya Taifa Endapo mtuhumiwa atakamatwa na raia, basi ni wajibu wa raia kumfikisha mtuhumiwa mbele ya kituo cha polisi haraka iwezekanavyo. 7
Haki ya Kupata Dhamana: Dhamana ni ruhusa anayopewa mtuhumiwa au mshitakiwa wakati akisubiri shitaka lake kupelekwa au kusikilizwa mahakamani au akisubiri hatma ya rufaa yake. Dhamana ni haki ya kila mtuhumiwa na huweza kutolewa na:- (i) Jaji au Hakimu (ii) Mkuu wa kituo cha Polisi. Kwa hiyo mara mtuhumiwa anapofikishwa kituo cha polisi au mahakamani ana haki ya kuomba na kupewa dhamana isipokuwa kwa makosa ya mauaji na uhaini. Mamlaka ya Jeshi la Polisi katika Mfumo Jinai Jeshi la polisi lina majukumu na mamlaka yafuatavyo; i. kulinda amani na utulivu katika nchi, ii. kuwatia nguvuni na kuwaweka watuhumiwa chini ya kizuizi (mahabusi), iii. kuwafikisha watuhumiwa mahakamani, iv. kupepeleza mashauri ya watuhumiwa, v. kutoa ushahidi mbele ya mahakama dhidi ya watuhumiwa wa makosa ya jinai, na vi. kusaidia katika majanga ya kitaifa. Haki za Msingi kwa Raia Katika Makosa ya Jinai Kila raia au mtuhumiwa ana haki mbele ya vyombo vya dola kama ifuatavyo: i. kila mtuhumiwa ana haki ya kuthaminiwa utu na heshima yake au kutoteswa pale anapotiwa nguvuni; 8
ii. kila mtuhumiwa ana haki ya kuelezwa kosa alilotenda kabla ya kukamatwa; iii. kila mtuhumiwa ana haki ya kupewa ushauri wa kisheria; iv. Ana haki ya matibabu pale anapokuwa ameumizwa au anaumwa; v. Ana haki ya chakula na malazi; vi. Ana haki ya kuwasiliana na ndugu zake; vii. kila mtuhumiwa ana haki ya kukaa kimya mpaka pale anapo hitaji huduma ya kuwakilishwa; viii. kila mtuhumiwa ana haki ya kupata dhamana isipokuwa kwa makosa yasiyokuwa na dhamana; ix. kila mtuhumiwa ana haki ya kuyafahamu mashitaka yake; x. kila mtuhumiwa anahesabiwa kuwa hana hatia hadi hapo chombo chenye mamlaka (mahakama) ya kuzisikiliza tuhuma kitakapomsikiliza na kumuona na hatia dhidi ya kosa analotuhumiwa. xi. Kila mtuhumuwa atachukuliwa kuwa mwenye akili timamu katika sheria ya makosa ya jinai hadi hapo itakapothibitishwa vinginevyo mbele ya sheria. Taratibu za Kukamatwa na Kuendesha Mashauri ya Jinai Taratibu za kukamata hadi kuendesha mashitaka husimamiwa na Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya Mwaka 1985 (Sura ya 20) na sheria nyingine kulingana na kosa la jinai. Hatua ya kukamatwa hadi adhabu hupitia hatua zifuatazo: 9
i. Kukamatwa kwa Mtuhumiwa ii. Upelelezi wa Makosa ya Jinai iii. Upelekaji wa Mashauri ya Jinai Mahakamani iv. Uendeshaji Mashauri ya Jinai Mahakamani v. Dhamana vi. Ushahidi Mahakamani vii. Hukumu itolewayo na Mahakama viii. Adhabu ix. Rufaa Jinsi ya Kumtia Mtu Nguvuni Mtuhumiwa atatiwa nguvuni na polisi au na mtu mwingine kwa kitendo cha kumgusa bega, mkono au kwa kumzuia kuondoka kwenda sehemu anayotaka. Kama mtuhumiwa atakaidi kutiwa nguvuni, au anatumia nguvu, au akitaka kutoroka basi njia yeyote halali na ya kufaa, kulingana na mazingira itatumika kumtia nguvuni. Wakati wa kumkamata mtuhumiwa, hatakiwi kuteswa au kuwekwa kwenye mazingira au hali ngumu zaidi ya kumzuia asitoroke. Ni muhimu kutambua kwamba askari polisi au mtu yeyote anayekamata anatakiwa ajitambulishe kwa mtuhumiwa kwa kutaja Jina Lake, hata kituo anachofanyia kazi na kutoa kitambulisho cha kazi. Matumizi ya Nguvu au Silaha Katika Ukamataji Askari polisi au mtu yeyote anayekamata mtuhumiwa haruhusiwi kutumia nguvu au/na silaha, au kumdhalilisha 10
mtuhumiwa zaidi ya kuhakikisha kwamba anamkamata na anamzuia kutoroka. Hivyo, askari polisi haruhusiwi kufanya jambo lolote ambalo linaweza kusababisha maumivu, majeraha makali na hata kifo kwa mtuhumiwa isipokuwa kama itaonesha na yeye kuamini kwa dhati kwamba kwa kufanya hivyo atakuwa amelinda na kuhifadhi maisha au kuzuia madhara makubwa kwa binadamu. Wajibu wa Mtuhumiwa Wakati wa Kukamatwa a. Kutii sheria pasipo shuruti; b. Kutii amri halali ya polisi wakati anatiwa nguvuni. c. Kujibu maswali atakayoulizwa na polisi au mtu yeyote anayemkamata. d. Kutoa taarifa sahihi ambazo atatakiwa kutoa mbele ya askari polisi au mtu yoyote anayemkamata zinazohusiana na kutendeka kwa kosa la jinai au kushiriki kwake katika kosa la jinai. e. Kutoa ushirikiano mbele ya polisi. Haki za Mtuhumiwa Wakati wa Kukamatwa a. Kumtaka mtu anayemtia nguvuni ajitambulishe kwa jina, cheo, sehemu anayofanyia kazi na sababu za kumkamata, b. Kutumia lugha inayofahamika kwa mtuhumiwa katika kueleza sababu za kutiwa kwake nguvuni. c. Kutoteswa, kupigwa au kufanyiwa unyanyasaji wa aina yeyote wakati akiwa mikononi mwa polisi au 11
mtu aliyemkamata wakati ametii amri. d. Kupewa nafasi ya kutoa taarifa kwa mwanasheria wake, ndugu au jamaa zake kuhusiana na kutiwa kwake nguvuni. e. Kutonyang anywa mali zake halali wakati wa kutiwa nguvuni au baada ya kutiwa nguvuni. f. Kupatiwa matibabu kama ni mgonjwa au ameumia wakati wa zoezi la ukamataji. g. Kupatiwa dhamana toka kwa polisi kabla hajafikishwa mahakamani kwa makosa yanayodhaminika. h. Kukaa kimya. UPEKUZI Upekuzi Sheria inampa polisi mamlaka ya kufanya upekuzi katika nyumba za kuishi watu, ofisi, magari, vyombo vyovyote au maeneo yeyote kama atakuwa na sababu za msingi kufanya hivyo. Hati ya Upekuzi Mkuu wa kituo cha polisi chochote ndiye mwenye mamlaka ya kutoa hati ya upekuzi ili kuruhusu zoezi la upekuzi kufanyika. Jinsi ya Kufanya Upekuzi Upekuzi wowote chini ya sheria hutakiwa ufanyike kwa mujibu wa vigezo, hali na mazingira yafuatayo: 12
a. Ulazima wa kuwa na hati ya upekuzi. b. Kufanyika kwa upekuzi bila hati ya upekuzi pale ambapo sheria inatoa mwanya kutokana na mazingira. Kwa mfano, mtuhumiwa kuaminika kuwa ana silaha au kitu chochote kinachohatarisha usalama na amani kwa umma. c. Kufanyika kwa upekuzi nyakati za mchana yaani kati ya jua kucha na kupwa (kati ya mawio na machweo). Hata hivyo upekuzi unaweza kufanyika muda mwingine wowote kama mahakama imetoa idhini ya kufanya hivyo. d. Kufanyika kwa upekuzi mbele ya mashahidi ambao wanaweza kuwa: kiongozi wa mtaa au shina au mtu mzima yeyote mwenye akili timamu. e. Kama itatokea kuna vitu au mali imechukuliwa kwa ajili ya ushahidi, basi ni lazima iandikishwe na mhusika au mwenye mali kutia sahihi kuthibitisha kutwaliwa kwa mali hizo. f. Kutunzwa katika sehemu salama vitu au mali zilizochukuliwa kabla ya kurejeshwa kwa mmiliki halali. Upelelezi au Uchunguzi wa Makosa ya Jinai Upelelezi wa makosa ya jinai hufanywa na jeshi la polisi kupitia askari maalumu wenye utalaamu wa kufanya kazi hiyo. Katika hatua hiyo askari polisi wanayo mamlaka ya kufanya mahojiano na kupata habari kuhusiana na kutendeka kwa kosa la jinai. 13
Kiutaratibu, mahojiano hufanyika kwa mdomo na kunakiliwa kimaandishi, na baada ya mahojiano mtoa maelezo anapaswa kutia sahihi yake kwenye maelezo hayo baada ya kuridhika na usahihi wa maelezo aliyotoa. Endapo maelezo yaliyotelewa yanaendana na kutendeka kwa kosa basi maelezo hayo pamoja na mtoa maelezo yatatumika katika ushahidi upande wa mashitaka pindi shauri hilo litakapofikishwa mahakamani. Haki za Mtuhumiwa Wakati wa Mahojiano Zifuatazo ni haki za mtuhumiwa wakati wa mahojiano mikononi mwa askari polisi; a. Kupata utambulisho kutoka kwa askari polisi anayefanya mahojiano. Hii ni pamoja na kuelezea jina, cheo chake na sababu za kutiwa nguvuni. b. Kuelezwa kwa lugha fasaha inayoeleweka kwa mtuhumiwa. c. Kupata tahadhari kutoka kwa askari polisi anayehoji kwamba hawajibiki kujibu maswali yote isipokuwa yale yanayohusu maelezo binafsi (wasifu wake) na jina lake. Hivyo mtuhumiwa ana haki ya kutojibu. d. Kuwasiliana na mwanasheria wake au ndugu zake akiwa mikononi mwa polisi, isipokuwa kama kuna sababu ya msingi ya kuzuiliwa asiwasiliane na hao wahusika. e. Kuthaminiwa utu wake pamoja na haki zake za binadamu. f. Kupatiwa matibabu anapokuwa yu mgonjwa au amejeruhiwa katika hatua za ukamataji. 14
DHAMANA Dhamana Kutoka Polisi Askari polisi wanayo mamlaka kutoa dhamana kwa mtuhumiwa kuwa nje ya kizuizi. Vigezo vifuatavyo hutumika kutoa dhamana; a. Uhakika wa mtuhumiwa kufika mahakamani siku atakayotakiwa kufanya hivyo. Katika kujiridhisha na kigezo hiki, askari polisi huzingatia yafuatayo; i. Historia ya maisha ya mtuhumiwa na mahusiano yake na jamii au, ajira yake ii. hali ya familia yake, na iii. kumbukumbu/rekodi au habari za maisha yake toka kwa polisi. b. Mazingira ya kosa au tuhuma. c. Maslahi ya mtuhumiwa, yaani: i. Kipindi atakapotakiwa kukaa mahabusu kama dhamana itakataliwa ikiwa ni pamoja na mazingira ya mahabusu penyewe, ii. Mahitaji au haja ya mtuhumiwa kuwa nje kwa lengo la kuandaa utetezi wake au kufika kwake mahakamani, ikiwa ni pamoja na kupata ushauri wa kisheria na uwakilishi mahakamani, iii. Mahitaji ya kiusalama ya mtuhumiwa ambayo yanaweza kutokana na ulevi wa kupindukia, majeraha au matumizi ya madawa ya kulevya, d. Usalama wa jamii hasa uwezekano wa mtuhumiwa kuharibu ushahidi kwa kuwatisha mashahidi au kuwazuia polisi kufanya upelelezi. 15
Hata hivyo, dhamana inayotolewa na jeshi la polisi haihusiani na kuweka dhamana mali au pesa zake na inaweza kuambatana na masharti yafuatayo: a. Mtuhumiwa kujidhamini kimaandishi au kuthibitisha kwa maandishi kwamba atafika mahakamani siku na muda uliopangwa. b. Mtuhumiwa kuhakikisha kimaandishi kwamba atazingatia na kufuata masharti ya dhamana atakapokuwa nje. c. Mtu mwingine anayeaminika mbele ya askari polisi anaweza kumdhamini mtuhumiwa. d. Uwezo wa mtuhumiwa au mdhamini kulipa kiasi cha fedha endapo mtuhumiwa atashindwa kufika mahakamani siku iliyopangwa kusikiliza shauri lake. Kama itatokea askari polisi kukataa kutoa dhamana kwa mtuhumiwa basi watatoa sababu za kukataa kimaandishi. Hali kadhalika, endapo askari polisi watakuwa wametoa dhamana lakini mtuhumiwa akashindwa kutimiza masharti ya dhamana, wanayo wajibu wa ya kumfikisha mtuhumiwa mahakamani haraka iwezekanavyo. Kufutwa kwa Dhamana ya Polisi Dhamana ya polisi inaweza kufutwa na mkuu wa kituo cha polisi husika kama itathibitika kwamba; a. Mtuhumiwa haonekani, yaani mtoro au; b. Ameshindwa au anaelekea kushindwa kuzingatia masharti ya dhamana. 16
Mtuhumiwa anayevunja kwa makusudi masharti ya dhamana akiwa nje kwa dhamana anakuwa ametenda kosa la jinai na akipatikana na hatia atawajibika kutumikia adhabu ambayo si zaidi ya adhabu ya kosa aliloshitakiwa nalo awali kabla ya kuvunja masharti ya dhamana yake. KUFIKISHWA MAHAKAMANI Mtuhumiwa Kufikishwa Mahakamani Mashitaka au shauri la jinai linaweza kufikishwa mahakamani na: a) Mtu Yeyote Mtu yoyote anayeamini kwamba mtu fulani ametenda kosa la jinai, anaweza kufikisha malalamiko hayo mahakamani. Hakimu ambaye malalamiko yatafikishwa kwake anatakiwa kutayarisha hati ya mashitaka au kuelekeza kuandaliwa kwa hati ya mashitaka na polisi au chombo chenye mamlaka ya kuandaa hati ya mashitaka. b) Chombo cha Dola Askari polisi au chombo chochote cha dola chenye mamlaka kama TAKUKURU kinawajibu kuandaa hati ya mashitaka na kumfikisha mahakamani mtuhumiwa aliye chini ya ulinzi wake. 17
Hati ya Mashitaka Hati ya mashitaka lazima iwe na taarifa zifuatazo kulingana na sehemu husika: a. Maelezo binafsi ya mtuhumiwa kama vile jina, umri, kabila, eneo analoishi, kazi au shughuli anayofanya. b. Kosa analoshitakiwa chini ya kifungu na sheria husika c. Maelezo ya kitendo au mazingira ya kosa lilivyotendeka kama vile mahali, muda na maelezo mengine ambayo yatafafanua mazingira ya kutendeka kwa kosa. d. Jina, sahihi na cheo cha mtu aliyetayarisha hati ya mashitaka. 18
Kubadilishwa kwa Hati ya Mashitaka Mahakama ina mamlaka ya kuamuru kubadilishwa kwa Hati ya Mashitaka pale itakapoona inafaa, kabla ya hukumu haijatolewa katika mazingira yafuatayo; a. baada ya pande zote kusikilizwa na mahakama, au b. pale upande wa mashitaka unapoona kwamba kuna ushahidi mpya dhidi ya mshitakiwa, au c. upande wa mashitaka unapoona kwamba ushahidi ulionao kwenye kosa husika hautoshi ila unaweza kuthibitisha kosa lingine dogo. Mshitakiwa ana haki ya kukiri au kukana mashitaka mapya baada ya kubadilishwa kwa hati ya mashitaka. Kwa hali hiyo, mtuhumiwa ana haki ya kuomba na kupata nakala ya Hati ya Mashitaka ili aweze kuelewa mashitaka dhidi yake na kupata msaada wa kisheria. Dhamana ya Mahakama Kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 1985, mtuhumiwa au mshitakiwa ana haki ya kupata dhamana isipokuwa katika makosa yafuatayo; a. Mauaji; b. Uhaini; c. Wizi wa kutumia silaha kubwa za moto; d. Kufanya biashara ya madawa ya kulevya ambayo yametajwa katika sheria ya Kuzuia Madawa ya Kulevya. Hii ikiwa ni pamoja na madawa ya unga aina ya cocaine. Hata hivyo, mahakama inamamlaka ya kutoa au kuzuia 19
dhamana katika shitaka lolote kulingana na hali ya shitaka na mazingira ya usalama wa mtuhumiwa katika jamii. Mazingira hayo ni kama; a. itathibitika kwamba mtuhumiwa amewahi kutumikia kifungo kinachozidi miaka mitatu. b. itathibitika kwamba mtuhumiwa amewahi kupewa dhamana lakini akakiuka masharti ya dhamana hiyo. c. mahakama itaona kwamba ni vema mtuhumiwa asipewe dhamana kwa sababu ya usalama wa mwombaji ama mlalamikaji. Dhamana inayotolewa na mahakama inaweza kuambatana na masharti yafuatayo; i. Kusalimisha hati ya kusafiria kwa polisi au vyombo vingine husika. ii. Kumzuia mtuhumiwa kusafiri nje ya eneo maalumu. iii. Kumtaka mtuhumiwa kuripoti kwenye kituo cha polisi kwa muda maalumu. iv. Kumzuia mtuhumiwa asionekana au kutembelea maeneo maalumu. v. Masharti mengineyo ambayo mahakama itaona inafaa. Jinsi ya Kutoa na Kupata Dhamana Kabla mtu hajapata dhamana lazima atimize masharti ya dhamana ambayo ni pamoja na a. Mdhamini wake au mtuhumiwa kusaini na kuingia 20
makubaliano na polisi au ofisi na Mkurugenzi wa Mashitaka, TAKUKURU au Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwamba atahudhuria mahakamani siku anayotakiwa. b. Mara baada ya kusaini au kuingia makubaliano hayo na vyombo husika kama ilivyoelezwa hapo juu basi mtuhumiwa atatoka kwa dhamana kama atakuwa yuko gerezani au mahabusu. Wajibu wa Mdhamini Ni wajibu wa mdhamini kuhakikisha kwamba mtuhumiwa au mshitakiwa anayedhaminiwa; a. anatimiza masharti ya dhamana na kuhudhuria mahakamani kama inavyotakiwa kufanya. b. endapo mtuhumiwa atakiuka masharti ya dhamana, na hasa pale anapotoroka, itabidi mdhamini kulipa kiwango cha dhamana alichojifunga. c. kuwa tayari kukamatwa kwa mali zake endapo mdhamini atashindwa kulipa kiwango cha fedha ya dhamana. d. ikiwa itashindikana kulipa kiwango cha dhamana kuwa tayari kuhukumiwa kutumikia kifungo kisichopungua miezi 6 (Sita). Mahakama kuu ina mamlaka ya kubadilisha masharti ya dhamana ambayo yamewekwa na Mahakama za chini na kumpa dhamana mtuhumiwa ambaye atakuwa amekataliwa dhamana na mahakama za chini. Kinachotakiwa ni kufikisha maombi hayo Mahakama Kuu yakiwa ni rufaa dhidi ya uamuzi wa mahakama za 21
chini kukataa kutoa dhamana au yakiwa ni maombi ya mapitio. USIKILIZAJI WA MASHITAKA Usikilizaji wa Mashitaka ya Jinai Mahakamani Katika mashauri ya jinai zipo pande tatu zinazohusika katika kuendesha na kusikiliza shauri. Pande hizo ni; a. Mahakama b. Mashitaka c. Utetezi wa Mashitaka a. Mahakama Upande wa mahakama huongozwa na hakimu pamoja na wasaidizi wake, mahakama huhusika na usikilizaji wa shauri na kisha kutolea maamuzi shauri lililo mbele yake kulingana na uzito wa ushahidi. b. Mashitaka Upande wa mashitaka ni Jamhuri, yaani Serikali na vyombo vyake ambavyo ni pamoja na Polisi, TAKUKURU, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali au taasisi yoyote yenye mamlaka ya kuendesha mashitaka, mwathirika wa kosa la jinai, pamoja na mashahidi watakaounga mkono mashitaka. c. Utetezi Upande huu unahusisha mtuhumiwa na mashahidi wake ambao watamsaidia katika utetezi wake kwa kukanusha 22
mashitaka dhidi yake. Kazi ya utetezi inaweza kufanywa na mtuhumiwa mwenyewe au wakili wake atakayempata kutoka kwa mawakili binafsi. Hatua za Usikilizaji wa Shauri la Jinai Katika kusikiliza shauri la jinai mahakamani upande wa mashitaka ndio wenye wajibu wa kuanza kwa kumsomea mshitakiwa shitaka linalomkabili kama lilivyoandaliwa kwenye hati ya mashitaka. Baada ya shitaka kusomwa mbele ya mshitakiwa, mshitakiwa hupaswa kujibu kwa ama kukiri kutenda kosa, au kukana kutenda kosa. Matokeo ya Kukiri Shitaka Mtuhumiwa akikiri kosa, hakimu atamuuliza mara kadhaa kuhakikisha kauli ya kukiri kisha atanukuu maneno ya kukiri kwa mtuhumiwa katika lugha nyepesi na fasaha ambayo inawakilisha kwa karibu sana yale aliyosema mtuhumiwa na kisha atamtia hatiani mtuhumiwa kwa kosa alilolikiri na kisha kutoa adhabu kulingana na sheria na taratibu za kimahakama. Matokeo ya Kukana Shitaka Mshitakiwa akikana shitaka lililosomwa mbele yake, mahakama itanukuu maneno ya kukana shitaka na kuutaka upande wa mashitaka kuendelea na mashitaka dhidi ya mshitakiwa ikiwa ni pamoja na hatua za kuita mashahidi na kutoa ushahidi kwa kadri ya mashahidi na ushahidi walionao. 23
KINGA DHIDI YA MAKOSA YA JINAI Kinga Dhidi ya Makosa ya Jinai Zipo kinga mbalimbali kisheria anazoweza kuzitumia mshitakiwa katika utetezi wa shauri la jinai. Kinga hizo ni pamoja na; i) Ugonjwa wa akili Tatizo la ugonjwa wa akili litakubalika ikiwa mtendaji alikuwa katika mazingira yafuatayo; a) alikuwa haelewi analolifanya wakati anatenda kosa la jinai. b) alishindwa kujitambua au kutambua kwamba hakupaswa kufanya yale aliyofanya. c) hakuwa na uwezo wa kuzuia au kudhibiti kosa lisifanyike. Mazingira ambayo utetezi huu au kinga hii inaweza kutumika katika shauri la jinai ni lazima kuwepo na ushahidi wa kuthibitisha kwamba mtuhumiwa alikuwa na matatizo ya akili wakati anatenda kosa hilo na si baada ya kutendeka hilo kosa. ii) Kutenda Kosa kwa Msukumo wa Ulevi Hali hii inaweza kuwa utetezi na kinga dhidi ya kosa la jinai endapo itathibitishwa kwamba wakati anatenda kosa alikuwa amelewa kwa kiwango cha kutoweza kujitambua au kutambua kama analolifanya ni kosa chini ya sheria. Utetezi huu utakubalika tu katika mazingira yafuatayo: a) Hali ya ulevi imetokea bila ridhaa ya mtuhumiwa 24
toka kwa mtu mwingine ambaye amemlewesha kwa hila na ulaghai. b) Kutokana na kuleweshwa akili za mtuhumiwa ziliathirika kiasi cha kutojitambua au kutotambua alilolifanya wakati anatenda kosa la jinai. iii) Umri Mdogo Chini ya Miaka Kumi Mtu yeyote aliye chini ya umri wa miaka 10 hawajibiki kwa tendo lolote la jinai analotenda na anakuwa hana hatia kwenye makosa yote ya jinai. Hali kadhalika mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka 12 yaani kumi na mbili au chini yake, hatakuwa na kosa la jinai kwenye makosa ya kujamiiana. iv) Haki ya Kujilinda au Kujihami Kila mtu anahaki ya kujilinda au kulinda mali yake au ya mdugu yake au rafiki yake kwa kutumia nguvu. Kwa hiyo, nguvu itakayotumika ni lazima iwe na uwiano na madhara yeyote dhidi ya mtuhumiwa. v) Kulazimishwa au Kushurutishwa Kutenda Kosa la Jinai Mtu yeyote hatawajibika kwa kutenda au kuacha kutenda jambo analodaiwa kutenda kisheria ikiwa amelifanya kosa husika chini ya kitisho cha kifo au kufanyiwa madhara makubwa dhidi ya maisha yake toka kwa watuhumiwa wenzake katika kosa hilo. vi) Kushitakiwa na Kuadhibiwa kwa Kosa Hilohilo Mtuhumiwa hatashitakiwa mara mbili baada ya 25
kutuhumiwa kwa kosa lilelile. vii) Kushitakiwa na Kuachiwa Huru Mtu hatashitakiwa kwa kosa ambalo alishashitakiwa kisha akaachiwa huru kwa kutopatikana na hatia au kwa sababu nyingine ya msingi itakayotolewa na upande wa mashitaka (nolle prosequi). viii) Mtuhumiwa Kutokuwepo Eneo la Tukio Mtuhumiwa atakuwa na kinga endapo atathibitisha mahakamani kwamba wakati kosa la jinai analoshitakiwa likitendeka hakuwepo kwenye eneo la tukio kwa sababu zozote zile ikiwa ni pamoja na safari au vinginevyo. ix) Kughadhabishwa au Kukasirishwa Kughadhabishwa au kukasirishwa kunakotokea wakati huo huo na kupelekea kutenda kosa la jinai wakati huo huo kunaweza kuwa utetezi na kinga katika makosa jinai na hivyo kupelekea kutuhumiwa kutenda kosa bila kukusudia au kutokukusudia kama: a) maneno yaliyotamkwa au kitendo kilichofanywa si kosa la jinai na ni halali kisheria. b) kosa la jinai lililofanywa linatokana na ushawishi, kusisimka na jazba ambazo zimetokana na mtu mwingine au matendo ya mtu mwingine. c) itathibitika kwamba kitendo hicho hakikuwa halali na ni kinyume cha sheria. x) Kuchukua au Kufanya Kitendo Dhidi ya Mali Halali Kuchukua au kufanya kitendo au kutokufanya jambo lolote kwenye kitu au mali yako halali toka kwa mtu 26
mwingine aliyenayo. Kitendo hicho lazima kifanyike bila udanganyifu au ulaghai wa aina yoyote. Mfano, kutuhumiwa kwa wizi wa radio wakati ambapo radio hiyo ni mali yako. Uamuzi wa Mahakama Baada ya kusikiliza mashahidi na ushahidi wa pande zote, mahakama itatoa uamuzi ambao ni ama; a. kumwachia huru mshitakiwa kwa kutokuwa na hatia, pale upande wa mashitaka unaposhindwa kuthibitisha mashitaka na utetezi wa mshitakiwa kukanusha mashitaka hayo. b. kumtia hatiani mtuhumiwa na kumhukumu kutumikia adhabu, kama upande wa mashitaka utathibitisha mashitaka dhidi ya mshitakiwa pasipo shaka yoyote na utetezi wake kushindwa kukanusha mashitaka hayo. Ombi la Kupunguziwa Adhabu Baada ya mahakama kumtia hatiani mshitakiwa, na kabla ya mahakama kutoa adhabu hutoa mwanya wa maombi kwa pande zote ya ama kupunguza adhabu au kutoa adhabu kama ilivyo kwenye sheria. Miongoni mwa sababu ambazo mahakama inaweza kuzikubali kupunguza adhabu ni pamoja na mshitakiwa kutenda kosa kwa mara ya kwanza, au ni mdhoofu wa ugonjwa ama umri mkubwa. Kadhalika, mojawapo ya sababu za upande wa mashitaka kuhakikisha mtuhumiwa anapata adhabu kali ni pamoja 27
na tabia ya mtuhumiwa kurudia rudia kosa husika ambalo ni kero katika jamii na kuwa kama fundisho kwa wengine. Adhabu Katika Makosa ya Jinai Baadhi ya adhabu ambazo Mahakama inaweza kutoa kwa mtu aliyepatikana na hatia katika shauri la jinai ni; i. Adhabu ya kifo kwa makosa ya mauaji, uhaini na kusababisha mgomo katika jeshi la wananchi. ii. Kulipa Faini iii. Kulipa Fidia iv. Kifungo cha Gerezani au cha nje v. Kuchapwa Viboko vi. Kutaifisha au kunyang anya mali vii. Kuwa chini ya matazamio ya kutotenda kosa ndani ya muda maalum viii. Kuwa chini ya Afisa Ustawi kwa kufanya shughuli za mafunzo maalum ix. Kutumikia jamii Rufaa, Marejeo na Mapitio Haki ya kukata rafaa, kuomba marejeo na/au kuomba mapitio ni haki ya kikatiba na kila mshitakiwa anastahili haki hiyo. Upande usiporidhika na maamuzi ya mahakama unayo haki ya ama kuomba kurudia kwa hukumu katika mahakama ileile; kukata rufaa au kuomba marejeo dhidi ya hukumu katika mahakama ya juu ya ile iliyotoa hukumu na yenye mamlaka ya kusikiliza rufaa au marejeo. 28
Tanganyika Law Society Plot No 391, Chato Street, Regent Estate P.O.BOX 2148, Dar es Salaam, Tel: +255222775313 Fax: +255222775314, Email: info@tls.or.tz, Website: www.tls.or.tz 30