HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA BENJAMIN WILLIAM MKAPA,KWA WANANCHI, 30 SEPTEMBA, 2001 Leo napenda nizungumze nanyi, kwa lugha nyepesi iwezekanavyo, juu ya mahusiano tunayowania kuyarekebisha kati yetu, tukiwa miongoni mwa nchi maskini, na mataifa tajiri yenye viwanda. Mahusiano nitakayoyazungumzia leo si yale ya misaada. Maana, nikiwa Rais wenu nafedheheshwa sana kuona bajeti yetu ya taifa inategemea mno wahisani. Pamoja na jitihada zote za kuongeza makusanyo ya kodi, bado tunaweza kugharamia asilimia 58 tu ya bajeti yetu kutokana na mapato ya ndani. Kwa maneno mengine, kwa kila shilingi mia moja kwenye bajeti yetu ya sasa, ni shilingi 58 tu ndizo zetu; shilingi 42 kwa kila mia ni misaada na mikopo kutoka nje. Wahenga walituasa: Mtegemea cha ndugu hufa maskini. Kazi mliyonipa, Ndugu Wananchi, ni kuweka misingi ya kulitoa taifa letu katika aibu hii ya utegemezi uliokithiri, ili serikali za nje, au taasisi yoyote ya nje, ikituvunjia heshima ya utu wetu na uhuru wetu, tuweze kuwajibu bila wasiwasi kuwa: Msitubabaishe, hatuli kwenu! Ili tufikie lengo hilo, tunapaswa kukuza uwezo wetu wa kuendelea kwa kujitegemea kwa kuongeza uzalishaji wa bidhaa bora, kwa bei nafuu, na kuziuza ndani na nje ya nchi kwa gharama nafuu. Tutafanya hivyo pia kwa kutoa huduma bora zaidi, ikiwemo za utalii, fedha, bima, usafiri na mawasiliano, nazo kwa ufanisi na kwa bei nafuu. Hakuna njia nyingine ya mkato katika vita dhidi ya unyonge wa umaskini. Nasisitiza umuhimu wa ubora wa bidhaa na huduma, kwa gharama nafuu, kwa sababu katika dunia ya utandawazi shughuli zote hizo hufanyika katika mazingira ya ushindani mkubwa sana; ushindani wa ufanisi, ushindani wa ubora, na ushindani wa bei. Kilicho bora na nafuu huuzika kwa wepesi zaidi. Huu ni ukweli wa dunia ya leo na ijayo. Kuupuuza ukweli huo ni kujichimbia zaidi kwenye lindi la umaskini. Ushindani mkali katika biashara, uwekezaji na huduma ni sura moja tu kati ya sura nyingi za dunia ya utandawazi; dunia ambayo haiwezekani tena kujitenga nayo au kukwepa maingiliano na nchi nyingine. Sura nyingine, ambayo ni dhahiri, ni kuwa kwenye ushindani huo mwenye nguvu zaidi aghalabu ndiye hushinda. Ukweli huo unabadilika tu iwapo upo utaratibu wa kutoa upendeleo fulani kwa mnyonge, ili kumwezesha mnyonge huyo, kwa misaada halisi, naye ajenge uwezo wa ushindani wa haki. Kila nchi maskini ina wajibu wa kuwa na sera muafaka kwa maendeleo na kujenga mazingira ya kisera, kisheria, kiutawala na kiutekelezaji yatakayokuza uzalishaji, huduma na biashara. Lakini hiyo peke yake haitoshi. Bado katika maingiliano ya kibiashara na kiuchumi na nchi tajiri tunahitaji upendeleo, na misaada halisi ya kujenga uwezo wa uzalishaji na biashara katika uchumi wa soko na mazingira ya ushindani. Mimi binafsi, na serikali yenu kwa jumla, tumekuwa mstari wa mbele katika kujenga hoja hizo kwa niaba ya nchi yetu sisi wenyewe, na kwa niaba ya nchi zote maskini, nyingi zikiwa barani Afrika. Tumekuwa hodari wa kujenga na kutetea hoja hizi kiasi kwamba tunaalikwa huku na huko kufafanua mikakati tunayoiona inafaa ili kuleta ushindani wa haki, ushindani wenye utu, katika dunia ya leo na ijayo; ushindani unaohakikisha nchi maskini nazo zinafaidika kutokana na maingiliano ya kibiashara na
kiuchumi duniani, kwa namna ambayo bado tunakuwa na uchumi wa kitaifa, uchumi unaokua, uchumi unaoleta maendeleo ya wote na kupunguza umaskini. Mfumo wa maingiliano ya kiuchumi na kibiashara duniani ambao hatima yake ni kuongeza umaskini wa walio maskini, badala ya kupunguza pengo kati ya matajiri na maskini, ni mfumo ambao Tanzania imeupinga, na itaendelea kuupinga, kwa nguvu zake zote. Ni kwa msingi huo Tanzania iliteuliwa kuwa mratibu wa nchi maskini zenye uwakilishi mjini Geneva kwenye Shirika la Biashara Duniani, (WTO). Kwa wadhifa huo, tuliandaa Mkutano wa Mawaziri wa Biashara wa Nchi Maskini mjini Zanzibar, tarehe 22 24 Julai mwaka huu. Nchi 45 kati ya 49 zilizoalikwa zilihudhuria mkutano huo, na kwa pamoja kupitisha Azimio la Zanzibar, pamoja na kukubaliana juu ya Ajenda ya Maendeleo na Malengo ya Majadiliano, kama maandalizi ya nchi maskini kwa ajili ya Mkutano wa Mawaziri wa Biashara Duniani utakaofanyika mjini Doha, nchini Qatar, mwezi Novemba mwaka huu. Kwa muda mrefu, nchi maskini zimejihisi kutosikilizwa vya kutosha katika majadiliano kuhusu mfumo wa biashara duniani, na ndio maana leo upo mfumo wenye madhara makubwa kwetu, mfumo ambao usipobadilishwa utatubakisha katika lindi la umaskini. Safari hii tunataka nchi tajiri zitusikilize vizuri zaidi, na kuzingatia hoja zetu, iwapo kweli wanaamini kuwa na sisi tunayo haki ya kunufaika na mfumo huo. Na kwa hili maneno yao hayatoshi; sasa tunataka vitendo. Maana, kama methali yetu isemavyo: Ada ya mja hunena, muungwana ni kitendo. Mojawapo ya mambo ambayo tunabishana sana na nchi tajiri ni juu ya umuhimu na uharaka wanaouona wao wa kuingiza mambo mapya kwenye makubaliano ya mfumo wa biashara duniani. Kimsingi sisi nchi maskini hatuoni mantiki ya kuongeza mambo mapya katika makubaliano yetu wakati ambapo yale tuliyokubaliana huko nyuma, hususan yale yenye maslahi kwa nchi maskini, bado hayajatekelezwa vya kutosha na nchi hizo tajiri. Aidha, nchi maskini zilitoa msimamo pale Zanzibar kuwa hazina uwezo wa kuingia kwenye majadiliano ya mambo mapya wakati ndio kwanza zinaanza kuelewa yale yaliyokubaliwa siku za nyuma. Hivyo, kwa maoni yetu, kinachohitajika hivi sasa si kukimbilia masuala na maeneo mapya, bali kusaidia nchi maskini kujenga uwezo wa kushiriki na kunufaika katika mfumo wa biashara uliopo duniani hivi sasa, kama wakubwa walivyotuahidi watafanya katika majadiliano na makubaliano ya awali. Mkutano wa Zanzibar, na mchango wa Tanzania, umesaidia kuelewesha wa nchi tajiri kuhusu hofu zetu za haki, na vipaumbele vyetu. Baada ya mkutano huo, Waziri wa Viwanda na Biashara wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alialikwa kwenye Mkutano wa Mashauriano wa Mawaziri wa Biashara kutoka nchi teule 18 duniani waliokutana Mexico tarehe 2 mwezi huu wa tisa. Tanzania ilialikwa kama mwakilishi wa nchi maskini, na kutokana na jukumu tulilochukua kuandaa mkutano wa Zanzibar. Itafanyika mikutano mingine ya maandalizi kabla ya mkutano wa Doha. Kote huko, Tanzania itakuwa mstari wa mbele kujenga hoja na kutetea maslahi ya nchi maskini kama yetu, ili hatimaye nasi tushiriki na kufaidika na mfumo wa biashara duniani, kwa manufaa ya wananchi wetu. Napenda muelewe kuwa kazi hii si nyepesi hata kidogo, maana tunataka kurekebisha mfumo ambao hivi sasa una manufaa kwa wakubwa, na wapiga kura wao.
Majadiliano haya yana sura ya uchumi, na yana sura ya kisiasa pia. Lakini ni kazi ambayo hatuna budi kuifanya. Bila hivyo nchi maskini kama yetu hazitainuka tena, hazitakuwa na uchumi wa kitaifa, hazitaendelea, na wala hazitashinda vita dhidi ya umaskini. Marekebisho haya ni kwa faida ya vizazi vijavyo vya nchi tajiri na nchi maskini. Maana, dunia ambayo siku hadi siku matajiri wanazidi kutajirika na maskini wanazidi kufukarika, daima haiwezi kutulia wala kuwa na amani. Pengine nitoe mifano ya jinsi ambavyo mfumo wa sasa unatukandamiza. Shirika la Umoja wa Mataifa la Biashara na Maendeleo (UNCTAD) limethibitisha hivi karibuni kuwa sababu kubwa ya bara la Afrika kutofaidika na biashara duniani ni kwa vile asilimia 80 ya mauzo yetu nje yanatokana na mafuta yasiyosafishwa na bidhaa za kilimo na madini zisizosindikwa. Katika soko la dunia, wakubwa ndio hupanga bei watakayonunulia bidhaa zetu hizo zisizosindikwa; kisha ni wao pia wanaopanga bei watakayotuuzia sisi bidhaa za viwanda vyao. Matokeo yake leo unahitaji kuuza kahawa, pamba, au korosho nyingi zaidi, pengine hata mara mbili au tatu, kupata fedha za kutosha kuagizia trekta moja kuliko ilivyokuwa miaka 10 au 20 iliyopita. Kwa nchi kama yetu, ambapo kilimo ndicho uti wa mgongo wa uchumi, hakuna njia nyingine ya kukihusisha kilimo na maendeleo ya uchumi kwa ujumla ila kwa kuongeza uwezo wetu wa kusindika mazao ya kilimo ndani ya nchi. Tukifanya hivyo, kutakuwa na uhakika wa soko na bei ya mazao ya mkulima; viwanda vya mazao ya kilimo vitatoa ajira kwa wanachi, ambao mapato yao yatajenga uwezo wa kununua bidhaa za viwanda vingine, ambavyo navyo sasa vitaajiri zaidi; na tutauza nje bidhaa zilizoongezewa thamani. Ndugu zangu, ukinunua kikombe cha chai au kahawa kwenye nchi tajiri, sehemu ya bei unayolipa inayomfikia mkulima wa Tanzania ni ndogo mno; ni utani, kama si kebehi. Sehemu kubwa ya bei inatokana na uongezaji thamani wa bidhaa zetu ghafi katika viwanda vya nchi tajiri, ikiwemo mishahara minono kwa wafanyakazi wa nchi hizo. Nitoe mfano. Bei ya kikombe kimoja cha kahawa bora, kama tuzalishayo sisi Tanzania, kwenye mgahawa wenye hadhi katika nchi tajiri, ni wastani wa sh. 1,800/= (USD 2), yaani karibu mara mbili ya wastani wa mapato ya mkulima wa Tanzania kwa siku. Katika miaka 20 iliyopita, bei ya kahawa tunayouza nje imepungua kwa wastani wa asilimia 225; lakini bei ya kahawa ya unga (instant coffee) katika nchi zilizoendelea na zinazosindika kahawa yetu imeongezeka kwa asilimia 200!! Tunapigana na umaskini katika mfumo wa mahusiano ya kibiashara duniani ambao ndani yake upo utaratibu wa unyonyaji, kiasi kwamba unavyozidi kuzalisha ndivyo mapato yanavyopungua. Kama nchi tajiri wanataka na sisi tufaidike, ili tushinde umaskini, lazima pamoja na mambo mengine watusaidie, katika uchumi wa soko, kujenga uwezo wa kusindika mazao yetu, na kuyaongezea thamani ndani ya nchi zetu maskini. Hivi sasa bei anayolipwa mkulima wetu haina uhakika, lakini bei ya bidhaa wanazotuuzia wao zina uhakika. Wakulima wao wanahakikishiwa mapato yao na Serikali kwa njia ya ruzuku au fidia. Hivi sasa, kwa mwaka, nchi tajiri duniani hutumia dola za kimarekani zaidi ya bilioni 300 (sh.270 trilioni) kuwapa ruzuku wakulima wao, kiasi ambacho ni karibu sawa na pato la mataifa yote ya Afrika kusini mwa jangwa la Sahara. Lakini, kwa vile sisi Serikali zetu hazina uwezo wa kutoa fidia au ruzuku, wakulima wetu wanaachwa wategemee huruma ya wanunuzi wakubwa wa kimataifa. Tunaambiwa bei ya kahawa imeshuka duniani, lakini ukienda Ulaya bei ya kahawa dukani au kwenye mgahawa ni ile ile. Vivyo hivyo kwa korosho, nguo za pamba na kadhalika. Tunajadiliana na kujenga hoja ana kwa ana na nchi tajiri kuwa kama kweli zinaunga mkono vita vyetu dhidi ya umaskini, na kama zinataka na sisi tufaidike na
mfumo wa biashara duniani, lazima wasaidie kufidia hasara za wakulima wetu pale bei ya mazao yao inaposhuka ghafla kwenye soko la kimataifa. Lazima pia uwepo uwiano mzuri baina ya bei ya tunachouza sisi, na kile wanachotuuzia wao. Takwimu za Shirika la UNCTAD zinaonyesha kuwa uwiano huo ungekuwepo, katika miaka 20 iliyopita Afrika ingekuwa imeuza mara mbili ya thamani ya mauzo yetu katika biashara ya kimataifa hivi sasa, na kuongeza wastani wa kipato cha mwaka kwa kila Mwafrika kwa asilimia 50; yaani pale ambapo kipato hicho hivi sasa ni sh.200,000/=, kipato hicho kingekuwa sh.300,000/= kama uwiano wa bei za mauzo yetu na manunuzi yetu nje ungebakia kama ulivyokuwa mwaka 1980. Ni dhahiri basi kuwa kama kweli nchi tajiri zinataka tufanikiwe katika vita dhidi ya umaskini, lazima watusaidie tutendewe haki zaidi kwenye soko la kimataifa, na uwepo uwiano wa haki kati ya bei ya tunachouza sisi na bei ya wanachotuuzia wao. Mfumo unaofanya kile sisi tunachowauzia wao kiendelee kushuka bei, lakini kile wao wanachotuuzia sisi kiendelee kupanda bei, ni mfumo ambao hauwezi kutetewa, maana si wa haki hata kidogo, na kwa kweli ni wa unyonyaji. Kukosekana kwa uwiano huo kumesababisha nchi za Kiafrika kuwa na uwezo mdogo zaidi wa kuwekeza kwenye huduma muhimu za jamii, kama vile afya na elimu, na katika kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara. Kisha uduni wa elimu, na mazingira yasiyofaa ya uwekezaji na biashara, hutumika kama sababu ya kuzidi kukwepa bara la Afrika. Ukichanganya hasara itokanayo na kukosekana kwa uwiano mzuri wa kibiashara, tatizo la madeni, na mambo mengine, utagundua kuwa badala ya mataifa tajiri kuisaidia Afrika, bara letu maskini ndilo linapeleka nje fedha nyingi zaidi kuliko zinazoingia. Inakadiriwa kuwa kwa kila shilingi 100 za fedha halisi zilizoingia barani Afrika kutoka nje tangu mwaka 1980, shilingi 106 zilitoka nje; shilingi 51 kutokana na uwiano mbaya wa biashara, shilingi 25 kutokana na ulipaji wa madeni na faida ya wawekezaji kutoka nje, na shilingi 30 kutokana na sababu nyinginezo zitumiwazo kutoa fedha nje. Matokeo yake tukipata sh.100, tunalipa sh.106. Tutaendelea kweli hivyo? Tunawahoji wakubwa: hawaoni ukweli huo? Ndugu Wanachi, Hatulalamiki tu. Nchi nyingi barani Afrika zimejitahidi sana kuzingatia ushauri wa wakubwa, ikiwemo kwa kulegeza masharti ya biashara na kufungua milango ya uwekezaji na biashara. Wakubwa walituahidi kuwa tukifanya hivyo watatusaidia, na pia tutafaidika na mfumo huo mpya wa biashara duniani. Lakini ukweli ni kuwa nyingi ya ahadi zao hazijatekelezwa, au ukipewa kwa mkono mmoja utanyang anywa kwa mkono mwingine. Ninyi Watanzania wenzangu mlishuhudia sakata la minofu ya samaki kutoka Ziwa Victoria ambapo kwa miezi 11 tulizuiwa kuuza barani Ulaya kwa kudhaniwa tu kuwa samaki wetu wana sumu, jambo ambalo lilikuja kuthibitika kuwa si kweli, lakini baada ya kutuletea hasara kubwa sana. Kwa vile minofu hiyo ndiyo zao letu kuu hivi sasa tuuzalo katika masoko ya Ulaya, kwa kipindi tulichozuiwa kuuza hasara tuliyopata inakadiriwa kufika Sh 24 bilioni fedha za kigeni, licha ya maelfu ya familia zinategemea biashara ya samaki hao kukosa mapato kwa kipindi hicho. Ukweli ni kuwa pamoja na ahadi nyingi za wakubwa, bado bidhaa za nchi maskini, ikiwemo zitokanazo na kilimo, hasa zilizosindikwa kama vile nguo na viatu, bado zinawekewa vizingiti vingi sana kuingia kwenye masoko ya wakubwa. Na haya si maneno yangu tu; wenyewe pia wanakiri hivyo. Katika mkutano wa kila mwaka wa mataifa makubwa (G8) uliofanyika mjini Genoa, Italia, mwezi Julai mwaka huu, ilitolewa taarifa kuhusu fursa na hatari za soko la utandawazi kwa nchi maskini. Taarifa hiyo iliandaliwa kwa pamoja na Benki ya Dunia,
Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), na Benki za Maendeleo za Kanda za Afrika, Asia, Ulaya, na Marekani. Napenda ninukuu taarifa hiyo ilivyosema kuhusu hali ngumu inayolikabili bara la Afrika. Ibara ya 26 ya taarifa hiyo inasema ifuatavyo: Isitoshe, Afrika inakabiliwa na ulindwaji wa hali ya juu sana wa masoko ya nchi tajiri (Afrika) inapotaka kuuza katika masoko hayo... Iwapo vikwazo viwekwavyo kwa bidhaa za Afrika katika masoko ya Kanada, Jumuiya ya Ulaya, Japan na Marekani vingefutwa, mauzo nje ya bara la Afrika ya bidhaa ambazo hazitokani na mafuta yangeongezeka kwa asilimia 14. Inakadiriwa pia kuwa, Afrika ingeruhusiwa kuuza bidhaa za kilimo kwa wingi zaidi kwenye soko la nchi hizo tajiri, mapato halisi barani Afrika yangeongezeka kwa USD 6 (Sh.5,400) kwa kila mtu Kwa hiyo, ni muhimu sana kwa nchi tajiri kupunguza kinga waliyojiwekea dhidi ya bidhaa za Afrika, hasa bidhaa za kilimo, ili kusaidia uchumi wa nchi za Kiafrika ukue kwa namna itakayosaidia kupunguza umaskini... 11 Tunafurahi wakubwa wanakiri hivyo; tunachodai na kushinikiza sasa ni kuwa watekeleze kwa vitendo ahadi zao za kurekebisha hali hiyo. Tulijifunza tangu enzi za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius K. Nyerere, kuwa chimbuko la sera ya nje ni sera za ndani. Sera za usawa ndani ya nchi zinatusukuma kutafuta usawa katika mahusiano na nchi za nje. Aidha, utekelezaji wa sera ya nje hupata nguvu kwa wanaozisimamia kujua Watanzania wote ni wamoja, na wanaunga mkono yale wanayoyalenga katika sera yetu ya nje. Nimewaelezeni leo sehemu au sura moja tu ya sera yetu ya nje, nayo ni kutafuta haki, usawa na manufaa katika dunia ya utandawazi, na biashara za ushindani mkali kimataifa. Tunahitaji sana mitaji kutoka nje ya nchi; lakini mwisho wake lazima tuwe bado na uchumi wa taifa, na kuwa na haki ya kubuni na kutekeleza sera ya taifa ya uchumi na maendeleo. Tunajua hatuwezi kuendelea, na kushinda vita dhidi ya umaskini, bila uwekezaji mitaji wenye ufanisi, na kushiriki kikamilifu kwenye biashara ya nje. Lakini tunajua pia kuwa mfumo wa biashara uliopo hauna maslahi ya kutosha kwetu, na hauwezi kutusaidia kupiga vita umaskini. Na kweli tusipoangalia unaweza kutuzidishia umaskini. Tunaomba wananchi mtuelewe tunapoongoza mapambano ya nchi maskini kudai haki, maslahi na usawa zaidi katika mahusiano ya kibiashara na kiuchumi na nchi tajiri zenye viwanda. Kama nilivyosema, kazi hiyo ni ngumu, maana tunataka kubadili mfumo ambao ulivyo sasa unafaidisha wakubwa. Lakini baadhi yao wameonyesha nia njema, na kama nchi maskini tukisimama pamoja, kama tulivyofanya Zanzibar, wakubwa hao watatusikiliza, maana hoja zenyewe ni wazi, wenyewe wanazikiri, wanachohitaji ni msukumo na utashi wa kisiasa kutekeleza. Ni wajibu wetu kuchochea utashi wao huo kwa kujenga na kutetea hoja zetu. Sisi ndani ya nchi tumeazimia kwa dhati kupiga vita umaskini. Lakini ili tufanikiwe utashi huo wa ndani ya nchi lazima uungwe mkono na utashi nje ya nchi. Sera nzuri ndani ya nchi lazima ziungwe mkono na sera nzuri nje ya nchi. Na mazingira mazuri ndani ya nchi yanahitaji mazingira bora kwenye nchi tajiri vile vile ndipo tufanikiwe.
Mkereketwa mmoja wa maendeleo aliwahi kulinganisha mahusiano ya kiuchumi na kibiashara duniani na mchezo wa bao. Ili mchezo wa bao uendelee lazima hata yule mchezaji asiye mahiri sana naye ale kete kiasi fulani. Iwapo bingwa atakula kete zote peke yake, huo utakuwa mwisho wa mchezo. Tanzania, kwa niaba ya nchi 49 maskini duniani, ianawasihi wakubwa wakubali kuendeleza mchezo kwa kuhakikisha na sisi wadogo tunafaidika. Kwa pamoja, nchi maskini na nchi tajiri, tunaweza kukubaliana juu ya mfumo bora zaidi wa uchumi na biashara duniani wenye maslahi kwa washiriki wote. Tukiwa waratibu wa mtazamo wa nchi maskini, tutaendelea kupigania mfumo huo. Ninachoomba kutoka kwenu, wananchi, ni uelewa wenu wa hali halisi ilivyo, na kuunga mkono harakati za Serikali yenu za kurekebisha hali ilivyo sasa. Tukijua mko pamoja nasi, tutakusanya nguvu za kimataifa tukiwa kifua mbele. Mungu ibariki Afrika Mungu ibariki Tanzania Ahsanteni kwa kunisikiliza. 1. G8 Genoa Summit, A Globalized Market Opportunities and Risks for the Poor : Global Poverty Report, July 2001